skip to main  |
      skip to sidebar
          
        
          
        
TAHADHARI KWA WANAOPENDA KUNUNUA "MALAYA"......DODOMA WAMENASWA WAKIWA NA ARVAs

 
 
WANAWAKE
 watatu raia wa Rwanda wanaosadikiwa kuendesha biashara ya ukahaba mjini
 Dodoma wamekamatwa na kupewa siku tatu kuondoka nchini, huku wawili 
kati yao wakikutwa na vidonge vya kupunguza makali ya virusi ya Ukimwi 
(ARVs).
Kukamatwa kwa wanawake hao ambao ni Esperance Hagenimana 
(28), Vestina Zaninika (27) na Ziada Mukamurera (25), kunafuatia mmoja 
wao Esperance kwenda kutoa taarifa kituo cha polisi kuwa alikuwa 
ameibiwa fedha taslimu Sh 800,000 na hati ya kusafiria.
Lakini, 
Polisi walipofika nyumba ya kulala wageni waliyofikia iliyopo eneo la 
Area D walikuta wanawake wengine wawili ambao walikuwa wakikaa chumba 
kimoja na Esperance.
Uchunguzi wa Polisi ulibaini kuwa mwanamke huyo 
hakuibiwa na kubaini wote si raia wa Tanzania. Hata hivyo kilikosekana 
kifungu cha kuwashitaki ndipo waliamua kupeleka sakata hilo Uhamiaji ili
 liweze kushughulikiwa.
Kulingana na maelezo yao, Esperance 
alitangulia kuja nchini kisha kuwaita wenzake ambao ilikuwa ni mara ya 
kwanza kuja nchini, lakini hata hivyo alisema kuwa, kumekuwa na makundi 
ya wanawake kutoka Rwanda wanaokuja nchini kipindi cha Bunge na hata 
mwaka jana kuna kundi lilikuja wakati wa mkutano wa Halmashauri Kuu ya 
Taifa (NEC) ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Kulingana na uchunguzi 
uliofanywa na Uhamiaji, wanawake hao waliingia nchini na kujitambulisha 
kuwa walikuja Dodoma kufanya biashara ya vitenge, lakini hawakuwa hata 
na kitenge kimoja ambacho kingeweza kuwaonesha kuwa walikuwa wakifanya 
biashara hiyo.
Juhudi hizo za Uhamiaji zinadaiwa kuwafikisha hadi 
klabu moja maarufu ya usiku iliyopo eneo la Area D ambapo walinzi wa 
Kimasai walikiri kuwafahamu wanawake hao na walikuwa wakiwafuata nyumba 
ya wageni waliyofikia kama mtu alikuwa akiwahitaji na walikuwa na ni 
wateja wa klabu hiyo ya usiku.
Alipoulizwa kuhusu suala hilo, Naibu 
Kamishna wa Uhamiaji, Ofisa Uhamiaji Mkoa wa Dodoma, Norah Massawe 
alikiri kukamatwa kwa wanawake hao na polisi na kukabidhiwa Uhamiaji.
Alisema
 mwanzoni wanawake hao walidai kuwa walikuja Dodoma kwa ajili ya kununua
 vitenge kwa ajili ya biashara na waliposhikiliwa na Polisi kwa siku 
kadhaa waliomba kurudishwa nchini kwao.
Alisema wawili kati yao walikutwa wakiwa na vidonge vya ARVs, lakini haijafahamika moja kwa moja kama walikuwa wagonjwa au la.
“Siwezi
 kusema walikuwa ni makahaba bali wanahisiwa hivyo kutokana na biashara 
waliyosema wanafanya kutoeleweka na hata maelezo ya walinzi wa klabu ya 
usiku kuwa walitambuliwa kama wateja wao, kwa kweli hilo siwezi 
kulithibitisha,” alisema.
Aliwataka wananchi kuwa makini na watu 
wasiowafahamu kwani hivi sasa Mkoa wa Dodoma umekuwa na mwingiliano 
mkubwa wa watu hasa katika kipindi cha Bunge.
Mwandishi wa habari 
hizi, alimtafuta Mratibu wa Ukimwi Mkoa wa Dodoma, Audrey Njelekela 
ambaye alisema kuwa, wamekuwa wakitoa elimu kuanzia ngazi ya Mkoa hadi 
mtaa ambapo kuna timu ya Mkoa ya Ukimwi na hata kwenye halmashauri kuna 
waratibu ambao wamekuwa akitoa elimu juu ya masuala mbalimbali 
yanayohusu Ukimwi.
Alisema kuwa kwa sasa kiwango cha maambukizi kwa 
Mkoa wa Dodoma ni asilimia 2.9 kwa takwimu za mwaka 2011 na 2012 
ikilinganisha na takwimu za mwaka 2007 hadi 2008 ambapo kiwango cha 
maambukizi kilikuwa asilimia 3.3.
Alisema kuwa waratibu wa ngazi ya 
halmashauri wamekuwa wakitoa elimu juu ya kujikinga na maambukizi ya 
Ukimwi kwenye maendeleo mbalimbali ikiwemo klabu za usiku.
Alisema 
kwa kuwa kondomu zinasambazwa maeneo mbalimbali yakiwemo ya starehe ni 
vyema wananchi kuhakikisha wanazitumia. “Matumizi ya kondomu ni muhimu 
sana kwani maeneo ya klabu za usiku na maeneo mengine ya starehe watu 
wengi wanachukuana tu lakini wanakuwa hawafahamiani,“ alisema.
Alisema kuwa kutokana na mwingiliano mkubwa wa watu katika Mkoa wa Dodoma hasa kipindi cha Bunge, umakini zaidi unahitajika.